Wednesday, May 8

KATIKA MAHUSIANO LEO SOMA NJIA SAHIHI ZA KUISHI NA MPENZI WAKO HATA KAMA ANAWIVU MKUBWA KIASI GANI KWAKO usihisi anakuonea chukua hatua madhubuti!



Upo kwenye uhusiano na mtu mwenye wivu? Hapa namaanisha pale ambapo mwenzako anaonesha wivu sehemu ambayo hujafanya lolote la kumfanya apatwe na hali hiyo. Mara nyingi hutokea, wewe upo kamili lakini mwenzako ni roho juu!

Kama ndivyo, basi niseme kwa kifupi kwamba upo kwenye wakati mgumu. Wivu wa kupitiliza ni mbaya, unaweza kutawala sehemu kubwa ya uhusiano wenu, pia ukasababisha maumivu ndani ya hisia zako na hali ikizidi hujenga mazingira ya kukata tamaa.
Wivu ni mateso yenu wote wawili! Unapokuwa kwenye penzi na mtu mwenye wivu unaweza kujikuta unavunjika moyo wa kupenda, hofu na vitisho. Haya yote kwa pamoja huweka rehani mapenzi yenu na kama tayari ni wanandoa basi ni usumbufu mtindo mmoja.

Kwa kawaida kuna hali ya kuogopa na kuhisi unavunjiwa heshima pale mwenzako anapokuonea wivu. Unaweza kujiuliza: “Yaani ananiona mimi malaya sana? Kwanini haniamini?” Yote kwa yote, inakera unapokuwa unaonewa wivu bila sababu za msingi.
Kuna watu hutafsiri umakini wa mtu kwa mpenzi wake ni wivu. Mtu kumhoji mpenzi wake pale mambo yanapokuwa hayapo sawa, hiyo haiwezi kuwa maana ya wivu. Katika hili, ni vizuri ukajiangalia wewe mwenyewe kwanza na nyendo zako.

Tayari umegundua mwenzi wako ana wivu usio na msingi, kwahiyo hapa inashauriwa katika sayansi ya saikolojia kwamba wewe ndiye uwe wa kwanza kuonesha huruma, upendo na heshima ili kujenga mazingira ya kirafiki kati yenu. Mpe uhakika wa penzi lenu bila kuzingatia jinsi unavyokuboa.
Ni muhimu kila mmoja ajione yupo salama kwenye uhusiano. Hivyo basi, ili kukubaliana na hali iliyopo kwa lengo la kuendelea kujenga penzi lenye afya ni lazima kwanza ujiangalie. Je, kuna kitu unafanya ambacho kinamfanya mpenzi wako ahamaki na asikuamini?

Je, unamuonesha mapenzi yenye shere ndani yake? Unavaa nguo za mitego? Unajichanganya kujibu maswali anapokuuliza? Unauweka mwili wako isivyofaa mbele ya watu wa jinsia ya pili? Unarudi nyumbani umechelewa bila taarifa? Unajichanganya na jinsia nyingine bila kumjulisha mwenzako?
Unaficha simu yako ya mkononi? Unawasikiliza na kuwazingatia wengine kuliko mpenzi wako? Kama utajiuliza na kubaini moja kati ya maswali hayo limo ndani ya yale unayoyafanya dhidi ya mwenzako, basi ni vema ukabadilika kuliko kulaumu na kumshutumu kwamba ana wivu kupitiliza.
Linda penzi au ndoa yako. Simaanishi ubadilike ghafla, lakini unaweza kujipa kazi (assignment) ya vitendo vyako taratibu mpaka utakapojiona wewe mwenyewe kwamba unahitaji kubadilika ili kuendana na mwenzi wako. Kama upo kwenye ndoa hupaswi kuishi kama mseja.

Ikiwa hufanyi jambo lolote baya lakini mwenzi wako ana wivu si kitoto, pia njia ya kumtuliza ni rahisi. Muoneshe mahaba tele, pia vitendo vyako vithibitishe penzi lako kwake kiasi kwamba hata yeye mwenyewe akose sababu ya kukutuhumu.
Wakati anapokushambulia, nawe usihamaki badala yake umuoneshe hali ya kwamba unamuelewa kwa kile anachogomba, sura yako impe picha kuwa wewe ni rafiki bora. Umsikilize bila kuhoji na uelewe anachozungumza.
Kitu muhimu kufahamu ni kuwa watu wenye wivu mara nyingi wanakuwa na maumivu ya hisia (emotional pain). Wewe unapaswa kulijua hilo, kwahiyo cha kufanya ni kuhakikisha unatuliza wivu wa mwenzi wako. Ninyi ni wapenzi, kwahiyo ni lazima muwe na hisia za aina moja.

Dk. Frank Gunzburg ambaye ni mwanasaikolojia mwenye shahada ya uzamivu (Ph.D) katika makala yake ya How To Deal With A Jealous Spouse, anasema kwamba mara nyingi si rahisi mtu kuelewa hisia za mwenzake na kujituma kumuweka huru.

Hata hivyo, anashauri kuwa kila mtu lazima afanye kazi kuhakikisha uhusiano unadumu. Anasema: “Wivu ni asili ya mtu, kwahiyo ni lazima uheshimu hisia za mwenzako. Kama mwenzako ana wivu wa kupitiliza, chukulia ni kasoro unayoweza kuirekebisha.”

Kwa kupitia maandishi hayo ya Gunzburg, nami natoa mkazo kwamba kila mmoja ni lazima ashikilie uhusiano wake. Hapo juu nimekuelekeza cha kufanya. Achana na maneno ya “aah, huyu naye amezidi wivu.” Tambua kuwa sifa ya mtu bora kwenye mapenzi ni yule anayeweza kuvumilia mikikimikiki ya mwenzake na akadumu.

Pointi ya ziada ni kuwa ukiona mpenzi wako anakuonea wivu sana, ujue kwamba anakukubali, anakuona una mvuto kiasi kwamba mtu yeyote wa jinsia yake anaweza kukutamani, hivyo anahisi hayupo salama kwa maana anaweza kuporwa na ukaenda kwa mwingine.
Kwa mantiki hiyo anakupenda. Akikuonea wivu anakuwa anajenga mazingira ya kukubakiza kwenye himaya yake, hivyo unachopaswa kufanya si kumtenda visa. Heshimu hisia zake, na umfanyie yale yatakayompa uhakika wa penzi lako kwake, kwamba hauna mpango wa kumsaliti.

Ipo pointi ya ubabe, kwamba unakuwa bingwa wa kumhoji mwenzako lakini wewe hautaki uhojiwe. Kila saa vidole vinabofya simu ya mpenzi wako, kuangalia simu zilizopigwa na kutoka pamoja na SMS. Yako unaiminya kibindoni. Hii siyo ustaarabu!
Kuficha simu ni dalili kwamba unafanya mawasiliano yasiyo salama kwenye penzi lenu. Kujichanganya kujibu pia ni athari ya kukosa uaminifu. Kama unataka uheshimiwe, ni lazima na wewe umheshimu mwenzako.

No comments:

Post a Comment

Search This Blog